Pages

Ads 468x60px

Featured Posts

Saturday, January 19, 2013

MTAZAMO WA MDAU KUHUSU SUALA LA GESI MTWARA






 Na: Maggid Mjengwa,
Ndugu zangu,
Kwenye jamii yetu kuna mjadala wa gesi. Kila ninapoufuatilia mjadala huu naiona hulka ya baadhi ya viongozi wetu inavyodhihiri; kuwa wanachanganya siasa na gesi. Kuna hatari ninayoiona ya nchi kulipuka. Ni wanasiasa walioelekeza mjadala wa gesi ubebe sura ya kimaeneo na kikabila. Na nahofia si muda mrefu tusasikia dini nayo ikichanganywa na gesi. Hapa kuna tatizo kubwa. Kinachokosekana ni ufahamu wa jambo zima kuhusu rasilimali zetu za nchi na nani wa kumnufaisha.

Tumefika mahali Watanzania tumekuwa kama wale watu wanaogombania bakuli za supu kwa ng’ombe ambaye hajachinjwa, na pengine hajatolewa hata zizini. Fikiri kama ng’ombe atakata kamba au kutoroka zizini.
Tumefika mahali baadhi ya wanasiasa kwa kauli zao, wanawafanya Watanzania waamini kuwa neema ya gesi kwao itapatikana kesho au kesho kutwa. Si kweli. Kimsingi manufaa ya gesi hii, kama itasimamiwa vema, ni kwa watoto na wajukuu zetu. Hii si gesi yetu, ni ya vizazi vijavyo. Ujinga ni kutaka kuitumia gesi ya vizazi vijavyo kama karata kwenye siasa zetu za sasa za reja reja- retail politics. Ndio hii hatari ninayoisema ya kuchanganya gesi na siasa.
Ni dhahiri, kuwa muda wetu wa kuishi humu duniani ni mfupi sana. Tofauti na wanyama, binadamu katika maisha yetu ya duniani, tuna kawaida ya kufikiria hiba ya kuacha nyuma yetu, kwa familia zetu na kwa jamii tunayoishi.
Fikiri mtoto uliyemzaa akikuuliza; “ Mama/ Baba, ukiondoka hapa duniani ungependa tukukumbuke kwa yepi?
Hilo ni swali gumu kwa yeyote anayeulizwa. Majibu ya swali hili yanatusaidia kuelewa umakini wa anayejibu. Swali hili linahusu hiba ya mtu anayoiacha nyuma yake. Hiba ambayo angependa akumbukwe kwa kuhusishwa nayo, ni urithi. Wazungu wanaita “Legacy”.
Huko nyuma nimepata kutoa mifano kadhaa ya viongozi walioacha hiba nyuma yao, hiba njema na mbaya; kule Burkina Faso alitokea kiongozi kijana na mwanamapinduzi. Aliacha hiba njema ya kuenziwa ndani ya nchi yake, Afrika na duniani, aliitwa Kapteni Thomas Sankara.
Mwanamapinduzi huyu alikuja kuawa kwa kupigwa risasi na wapinga mapinduzi na maendeleo ya Burkina Faso. Sankara alipata kukaririwa akisema;
“Ningependa kuacha nyuma yangu, imani ya kuwa, kama tunaimarisha kiwango fulani cha uangalifu na oganaizesheni, basi, tunastahili ushindi. Kamwe huwezi kuleta mabadiliko ya kimsingi bila ya kuwa na kiwango fulani cha uwendawazimu.
Hali hii inatokana na kutoshinikizwa na taratibu zilizozoeleka, kuwa na ujasiri wa
kuzipa mgongo kanuni za kizamani, ujasiri wa kuanzisha mustakabali.
Ni wendawazimu wa jana waliotuwezesha kuyafanya tuyafanyao leo.
Ninataka kuwa mmoja wa wendawazimu hao.” ( Hayati, Kapteni Thomas Sankara)
Ndugu zangu,
Mara kadhaa nimemnukuu Mwandishi mahiri Frantz Fanon aliyepata
kusema; ”Kila kizazi kina jukumu lake. Kina lazima ya kutoka kwenye hali ya ugiza na kulitafuta jukumu lake; kulikamilisha au kulisaliti”-
(Frantz Fanon.) Ni sisi wenyewe ndio wenye kuandika historia yetu kwa kupitia
matendo yetu, na zaidi kupitia harakati zetu za mapambano dhidi ya maovu ya aina zote .
Kamwe hatuwezi kulikamilisha jukumu la kizazi chetu, jukumu la kujikomboa kiuchumi
kama tutaonyesha hofu ya kupambana na maovu katika jamii.
Tuwe tayari kujitoa muhanga. Kila mzalendo wa nchi hii apambane mahali alipo kwa
kutumia silaha iliyo karibu naye. Apambane kwa ajili ya Tanzania kama taifa. Ni jukumu la kizazi chetu
Katika mapambano haya, tusikubali matokeo mengine bali ni ushindi wa jumla. Na huko nyuma niliwahi kutoa mfano wa Ken-Saro Wiwa wa Nigeria. Ni mfano wa vijana wengi wa bara hili, vijana waliolitafuta jukumu la kizazi chao, wakalitekeleza, hawakulisaliti.
Kijana huyu alikuwa ni mwanaharakati wa haki za kimazingira. Aliwahamasisha watu wa
kabila la Ogoni, kuandamana na kupinga kampuni ya mafuta ya Shell BP ya Uingereza kupewa eneo kubwa la ardhi ya Ogoni ili waachimbe mafuta. Fedha zilizotokana na mafuta hayo ziliishia mifukoni mwa wateule wachache kule Lagos.
Watu wa Ogoni walibaki na ufukara wao na huku mazingira yao yakiharibiwa vibaya. Zaidi ya miaka kumi na sita iliyopita, Ken-Saro Wiwa na wenzake 17 walinyongwa na utawala wa kijeshi wa Nigeria.
Saro Wiwa alijitoa mhanga. Dunia ikafahamu madhira ya watu wa Ogoni. Mabadiliko
yakatokea. Saro-Wiwa na wenzake walikufa kwa ajili ya kizazi cha leo na
kesho cha Kabila la Ogoni na Wanaigeria kwa ujumla.
Ni heri kufa na kuacha fikra zinazoishi kuliko kuishi bila kufikiri. Nahitimisha.
0754 678 252/ 0788 111 765 http://mjengwablog.co.tz

Friday, November 2, 2012

ULINZI MKALI WATANDA KESI YA PONDA.

                                                                       

ULINZI wa aina yake uliwekwa katika mahakama ya Hakimu Mkazi, Kisutu Dar es Salaam jana wakati Katibu  wa  Jumuiya na Taasisi za  Kiislamu Tanzania, Sheikh, Ponda Issa Ponda alipofikishwa mahakamani hapo na watu wengine 49.
Ponda na wafuasi wake walifikishwa mahakamani hapo kusikiliza kesi inayowakabili ,wakidaiwa  kufanya vurugu na kuharibu mali.
Hata hivyo, wakati wafuasi hao wakiachiwa kwa dhamana, Mahakama hiyo ilisema kuwa haina mamlaka ya kisheria ya kutoa dhamana kwa Sheikh Ponda anayetuhumiwa kuchochea vurugu hizo.

Sheikh Ponda na wafuasi wake walifikishwa mahakamani hapo jana asubuhi chini ya ulinzi mkali. Katika viwanja vya Mahakama ya Kisutu pia kulikuwa na ulinzi mkali wa vikosi ya polisi pamoja na kuwekwa vyombo maalumu vya usalama vilivyotumika kuwakagua watu waliokuwa wanaingia hadi Ponda alipoondolewa kurudi rumande baada ya kesi kuahirishwa.
Mbali na wingi wa askari waliokuwa wakilinda usalama katika eneo la mahakama hiyo wakiwa na silaha, mbwa na farasi, pia jana kuliwekwa mashine maalumu ya ukaguzi kwa kila aliyekuwa akiingia mahakamani hapo pamoja na kifaa cha kutambua milipuko.
Mahakamani kulifungwa kamera maalumu za usalama(CCTV) kwenye lango kuu la kuingilia hapo.

Mahakamani
Washtakiwa hao walipandishwa kizimbani na Mwendesha Mashtaka, Wakili wa Serikali Mwandamizi (SSA) Tumaini Kweka ambaye baada ya kesi kutajwa alisema upelelezi wake umeshakamilika na kuiomba  mahakama ipange tarehe ya usikilizwaji wa awali.
Alisema siku hiyo washtakiwa hao watasomewa maelezo ya awali ya kesi inayowakabili na kutakiwa kubainisha mambo wanayokubaliana nayo na wasiyokubaliana nayo.
Hata hivyo, Wakili wa washtakiwa hao, Juma Nassoro, aliikumbusha mahakama kuhusu dhamana ya washtakiwa hao, akisema walipopandishwa kizimbani kwa mara ya kwanza, maombi yao ya dhamana hayakushughulikiwa kwa vile hakimu aliyepangwa kusikiliza kesi hiyo hakuwapo.
“Mheshimiwa hakimu, kwa kuwa leo upo mwenyewe, basi tunaomba uamuzi wa maombi ya dhamana kwa washtakiwa,”  aliomba Wakili Nassoro.
Hakimu anayesikiliza kesi hiyo, Victoria Nongwa alikubaliana na maombi hayo ya dhamana na kusema kuwa, dhamana iko wazi kwa washtakiwa wote isipokuwa mshtakiwa wa kwanza tu (Sheikh Ponda), ambaye dhamana yake imefungwa na DPP.
“Dhamana iko wazi kwa washtakiwa wa pili hadi wa 50 kwa kuwa makosa yao yanaweza kuwekewa dhamana, isipokuwa mshtakiwa wa kwanza tu, kwa sababu DPP alileta hati ya kuzuia asipewe dhamana,”  alisema Hakimu Nongwa na kuongeza:
“Hivyo mahakama hii haina uwezo wa kisheria kutoa dhamana kwa mshtakiwa wa kwanza mpaka hapo DPP atakapoleta hati nyingine ya kuondoa zuio la awali.”
Kwa washtakiwa wengine, Hakimu Nongwa aliwapa masharti ya dhamana, akiwataka kuwa na wadhamini wawili kwa kila mshtakiwa, wanaotambulika, wenye vitambulisho, na kwamba wote kila mmoja asaini dhamana ya Sh1 milioni.
Pia Hakimu Nongwa aliwaamuru washtakiwa hao wasiende katika eneo la mgogoro uliowasababishia kesi hiyo (Malkazi, Chang’ombe), hadi hapo kesi itakapokwisha.
Baada  ya kutoa masharti hayo ya dhamana, Hakimu Nongwa aliahirisha kesi hiyo hadi Novemba 15, kesi hiyo itakaposikilizwa katika hatua ya awali, na kwamba dhamana kwa washtakiwa hao itashughulikiwa kwa taratibu za kawaida kama ilivyo kwa washtakiwa wengine.
Alisema kuwa kila mdhamini anaweza kupeleka mahakamani barua yake ya udhamini wakati wowote, na kama atatimiza masharti hayo ya dhamana, mshtakiwa husika ataachiwa huru kwa dhamana.
Ulinzi mahakamani
Kutokana na kuwapo kwa kesi hiyo, kila mtu aliyekuwa anaingia mahakamani, alikaguliwa kwa kutumia mashine maalumu, huku kamera ikiwa imefungwa lango kuu kuhakikisha kuwa hali ya usalama na amani inatawala kabla, wakati na baada ya kesi hiyo kuisha.
Jumla ya magari saba yakiwa na askari polisi na askari Magereza, zaidi ya 50, waliovalia mavazi maalumu huku wakiwa  na mabomu ya machozi na bunduki, walikuwa wametanda katika eneo lote kuzunguka mahakama.
Pia lilikuwapo gari la maji ya kuwasha,  mbwa watano huku askari wengine wakifanya doria kwa kutumia farasi.
Hata hivyo, kesi hiyo ilisikilizwa mapema sana na kutokana na hali ya ulinzi na ukaguzi mkali uliokuwapo mahakamani hapo, watu wengine waliokuwa na ndugu zao hao waliofikishwa mahakamani hapo, hawakuruhusiwa kuvuka lango la mahakama.
Baada ya kesi hiyo kuahirishwa, ndugu na jamaa wa washtakiwa hao waliondoka  katika eneo la mahakama kwa makundi, huku askari wakiwasindikiza taratibu hadi walipotokomea.

Maoni

Wakizungumzia hali ya ulinzi huo, baadhi ya wadau wa mahakama walilipongeza Jeshi la Polisi kwa kuimarisha ulinzi kwa kiasi hicho mahakamani hapo na kushauri hali hiyo  iendelee katika kipindi hiki ambacho hali ya usalama ni tete.
Wakili wa Kujitegemea, Majura Magafu  aliiomba Serikali kuendeleza mfumo huo wa ulinzi katika mahakama zote kwa sababu hali ya usalama bado ni tete.
Naye Gray Hizza aliunga mkono kuwapo kwa  mfumo huo wa ulinzi  mahakamani  ili kukinga uwezekano wowote wa uvunjifu wa amani unaoweza kutokea kwa sababu eneo hilo ni sehemu muhimu ya watu kupata haki.
Ponda na wenzake walipandishwa kizimbani kwa mara ya kwanza Oktoba 18, 2012 chini ya ulinzi mkali, na kusomewa mashtaka matano yakiwamo wizi na uchochezi.
Tuhuma zingine ni kula njama, kuingia kwa nguvu kwenye eneo lisilo mali yake kwa nia ya kutenda kosa na kujimilikisha ardhi kwa nguvu na kusababisha uvunjifu wa amani.
Sheikh Ponda alifikishwa mahakamani hapo akiwa na watu wengine 49 ambao waliunganishwa naye katika mashtaka manne isipokuwa shtaka la uchochezi ambalo linamkabili Ponda pekee.
Kauli ya Pinda
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda alisisitiza kuwa Serikali itavisambaratisha vikundi vyote vinavyochochea vurugu nchini, kuwa itatumia kila njia kukabiliana navyo.
Pinda alitoa kauli hiyo jana wakati akijibu swali la Mbunge wa Nzega CCM, Dk Khamis Kingwangalla wakati wa maswali kwa Waziri Mkuu akitaka kujua Serikali inachukua hatua gani kuenzi amani baada ya kutokea vurugu za kidini nchini za kuchoma makanisa na kukojolea Quran.
Pinda alisema Watanzania waivumilie Serikali itakapokuwa ikichukua hatua kali dhidi ya vikundi vya dini ambavyo vinaendelea kuvuruga amani.
“Napenda kuwaomba Watanzania watuvumilie pale tutakapochukua hatua kali dhidi ya vikundi hivyo,” alisema.
Alisema anajua kuwa viongozi wa madhehebu ya dini wamekuwa wakikutana mara kwa mara kuzungumzia amani, hivyo aliwataka waongeze kasi zaidi ya kukutana.
Kigwangalla pia aliwataka Waislamu upande wao kutoa tamko kuhusu vurugu za kidini zilizotokea hivi karibuni kama walivyofanya maaskofu.
KamandaKova
Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alisema jana jioni kuwa Jeshi la Polisi limejipanga kwa yeyote atakayeanzisha vurugu leo.
Akizungumza na Mwananchi kwa simu, Kova alisema: “Tunafahamu wanaofanya hivi si wote Waislamu, nawasihi watu wasijihusishe na maandamano kwa kuwa ni haramu.
“Hakuna kibali kilichoombwa, hakuna ruhusa ya kuandamana na maandamano yoyote leo hayako  ndani ya sheria,” alisema Kova.

Friday, October 26, 2012

TUME: UAMSHO INATUMIWA NA WAHUNI

                                                                             


TUME ya Haki za Binadamu na Utawala Bora imesema wakati kuna madai kwamba Jumuiya ya Uamsho ni ya kidini (Kiislamu), lakini imekuwa ikitumiwa na makundi ya wahuni ambayo yamejipachika majina tofauti.
Taarifa ya Tume hiyo iliyotumwa kwa vyombo vya habari jana ikiwa imesainiwa na Kamishna wake, Zahor Khamis, imetaja baadhi ya majina ya makundi hayo kuwa ni Mbwa mwitu, Simba mkali, Ubaya ubaya na Toto tundu na kuongeza kuwa yamekuwa yakitumika kufanikisha azma yao.
Mbali na jumuiya hiyo kutumiwa na wahuni, Tume pia imesema kutekwa kwa kiongozi wa jumuiya hiyo, Shekhe Farid Hadi Ahmed, kuna utata mkubwa ambao unahitaji uchunguzi na ufafanuzi kufahamu huko alikotekwa na kutoa mfano wa madai ya kunyimwa kula kwa siku tatu bila kuathirika kiafya.
Tume hiyo imehoji kama kweli alikuwa ametekwa, aliwezaje kufika msalani ambako alikuwa akinywa maji, wakati alikuwa amefungwa kitambaa usoni na mikononi akiwa na pingu na ilikuwa nyumba ambayo haijui! Kutokana na utata huo, Tume imemtaka Shekhe Farid kutoa maelezo yanayothibitisha pasipo shaka ili kuwathibitishia Wazanzibari, Watanzania na ulimwengu kwa jumla, juu ya kutoweka kwake.
“Shekhe Farid amedai alitekwa na watu wasiojulikana tarehe 16 mwezi huu na kuonekana siku tatu baadaye akiwa katika hali ya uzima na salama jambo ambalo lilisababisha vurugu kubwa Zanzibar na kusimama kwa shughuli zote za kiuchumi na kijamii,” ilieleza taarifa hiyo ya Tume.
Kwa mujibu wa Tume, kutokana na fujo hizo zilizotokea, hasara ilitokea ambayo mpaka sasa haijajulikana thamani askari Polisi wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), Said Abdulrahman kuliuawa.
Kutokana na matukio hayo, Tume imeishauri Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, kuwatafuta na kuwakamata wote walioshiriki katika vurugu hizo na kuvunja vikundi vyote vya kihalifu vilivyoanza kushamiri Zanzibar.
“Tunalaani mauaji ya askari Abdulrahman kwani ni uvunjaji wa haki za biaadamu, inapingana na sheria za nchi na ni kinyume na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ibara ya 14 inayozungumzia haki ya kuishi na Katiba ya Zanzibar ibara ya 13 inayozungumzia haki ya kuwa hai,” taarifa hiyo ilifafanua.
Tume pia imelaani kitendo alichofanyiwa Diwani wa CCM Wadi ya Chumbuni kwa kushambuliwa na kujeruhiwa, kitendo ambacho kinakwenda kinyume na haki za binaadamu na Katiba ya Tanzania inayopiga marufuku mtu kuteswa, kuadhibiwa kinyama au adhabu za kumdhalilisha.
“Kuna uhusiano gani wa kutekwa kwa kiongozi wa Uamsho na hujuma za mali za watu na CCM?” Taarifa hiyo ilihoji. Kwa mujibu wa Kamishina wa Jeshi la Polisi Zanzibar Mussa Ali Mussa Polisi inafanya uchunguzi wa kina kubaini kama Shekhe Farid anahusika na mtandao hatari wa ugaidi wa Al-Qaeda.
Akizungumza na gazeti hili kwa simu jana, Mussa alisema Polisi nchini inafanya kazi hiyo kwa kushirikiana na taasisi za kimataifa ikiwamo Polisi - Interpol.
“Jeshi la Polisi nchini kwa sasa linafuatilia kwa karibu sana nyendo zote za kiongozi wa Uamsho Shekhe Farid ikiwamo kuhusishwa kwake na mtandao wa Al-Qaeda,” alisema.

IJUE MAANA YA EID EL HAJJ

SIKU ya leo wengi wetu tumezoea kuiita sikukuu kubwa tukisema ni siku ambayo wakubwa ndiyo wanapewa zawadi na pia tumezoea kusoma ni sikukuu ya Mfungo tatu.
Sikukuu hii kubwa ina majina mengi kiasi, ambayo ni Idd el Hajj yaani Idd ya Hijja; Idd al Adh-ha yenye maana sikukuu ya sadaka lakini pia inafahamika kama Idd la Kabir ambayo ni sikukuu kubwa. Sikukuu hii hupatikana katika mwezi huu wa kiislamu unaofahamika kama Dhul Hijjah ambao ni mwezi wa Hija na ni mtukufu.
Katika mwezi huu kuna siku 10 za mwanzo ambazo ni siku bora kabisa katika dunia na zina fadhila kubwa kutokana na aya na hadithi mbalimbali.
Miongoni mwa hadithi ni ile inayotokana na Ibn Abbas (Radhiya Lahu anhuma). Mtume wa Mwenyezi Mungu (S.A.W) amesema: “Hakuna siku ambazo vitendo vyake vyema anavipenda Allah kama siku kumi hizi (siku kumi za mwanzo wa mwezi wa Dhul-Hijja).
Akaulizwa je, hata Jihaad katika njia ya Allah? Akajibu “hata jihaad katika njia ya Allah isipokuwa mtu aliyekwenda na maisha yake na mali yake ikawa hakurudi na kimojawapo”.
Vitendo hivyo vyema vinavyotajwa ni pamoja na kutimiza Hijja na Umra kwa wenye uwezo; kuomba toba ya ukweli; Kufunga siku hizi hasa siku ya Arafah; kuzidisha vitendo vyema mbalimbali kama kuswali sunna zaidi, kusoma Kurani, sadaka, dua, kutii wazazi, kuwasiliana na jamaa, kufanya wema na jirani, kuambizana yaliyo mema na kukatazana yaliyo maovu, kufanyiana wema na ihsani na kuchinja baada ya swala ya Idd.
Pia kumkumbuka sana Allah (S.W) kwa Tasbih, Tahmid, Tahlil na Takbir ambayo ni “Allahu Akbar, Allahu Akbar, Laa Ilaha Illa Allaah Wa-Allaahu Akbar, Allahu Akbar Walillahil-hamd”.
Takbir inapaswa kusomwa wakati wote usiku au mchana tokea unapoingia mwezi wa Dhul-Hijja na inaendelea mpaka siku ya mwisho ya siku za Tashriq na pia baada ya kila swala na huanza asubuhi ya siku ya Arafat mpaka siku ya mwisho ya Tashriq .
Siku ya 11, 12 na 13 ya Dhul-Hijja yaani baada ya siku ya Idd zimeitwa siku za Tashriq kwa sababu watu walikuwa wakikatakata nyama na kuzianika juani. Pia siku hizi hujulikana kuwa ‘siku za Minaa’. Inatakiwa Wanaume waseme Takbir kwa sauti ili kuwakumbusha wengine kurudisha sunna ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (S.A.W) na wanawake waseme kimya kimya isipokuwa wakiwa na mahaarim wao.
Imesemekana kuwa ukiandama mwezi wa Dhul-Hijja Ibn ‘Umar na Abu Hurayrah walikuwa wakienda sokoni na kufanya takbir kwa sauti ili kuwakumbusha watu.
Nikirudia siku hii ya Idd ambayo huitwa ya sadaka ni kutokana na watu kutakiwa kuchinja mnyama kama mbuzi, ng’ombe au kondoo na kisha kutoa sadaka kwa masikini na pia kutumiwa katika familia na ndiyo sababu kwa watu waliokwenda Makka kuhiji kuchinja wanyama.
Baada ya kuchinja kama alivyoagiza Mtume Muhammad (S.A.W), mchinjaji anaamrishwa aigawe nyama mafungu matatu, fungu moja awape masikini na mafakiri , fungu la pili awape majirani na ndugu na lile la tatu ni lake na familia yake.
Uchinjaji huu ni kama kumbukumbu ya sadaka ya Nabii Ibrahim ambaye anatajwa kwenye Kurani na Biblia kuwa alikuwa tayari kumchinja mwanawe wa kumzaa Nabii Ismail kama kwenye Kuran au Isaka (Biblia) kama sadaka kwa Mwenyezi Mungu lakini Mungu alimzuia asimchinje na akampatia mwanakondoo badala yake.
Mafundisho yanatueleza kuwa malaika Jibril alimshika mkono nabii Ibrahim kabla ya kumchinja mtoto wake Ismail ikiwa ni ishara ya kumzuia kutenda tendo hilo na ndipo aliposhushiwa kondoo amchinje. Maelezo hayo yanapatikana katika Kurani kwenye sura ya al-Hajj aya ya 37 na Biblia katika kitabu cha Mwanzo sura ya 22 ambapo anatajwa kama Abraham.
Uchinjaji huo wa mnyama unafanyika baada ya swala ya Idd ambapo Allah (S.W) amesema katika suratul Kawthar 108:2 “Basi swali kwa ajili ya Mola wako na uchinje “. Ibada hii ya kuchinja ni sunna iliyosisitizwa hata na baadhi ya wanazuoni ambao wameona kuwa ni wajibu kwa kila aliyekuwa na uwezo.
Muislamu kabla ya kufikia hatua ya kuchinja anatakiwa kutia nia ya kuchinja, asikate nywele wala kucha mpaka amalize kuchinja. Kuna hadithi moja inasema: “Ukiandama mwezi wa Dhul-Hijja na ikiwa yuko anayetaka kuchinja basi asikate kucha wala nywele wala kutoa kitu katika ngozi yake mpaka akimaliza kuchinja”.
Idd husherehekewa kati ya tarehe 10 hadi 13 ya mwezi wa Dhul Hijjah wa kalenda ya Kiislamu. Tarehe halisi hutegemea kuonekana kwa mwezi. Kwa mwaka huu ndiyo siku ya leo ambayo ni siku nzuri ya Ijumaa. ]Sherehe za siku hii huanza kwa swala la Idd na baadaye kufuatiwa na baraza la Idd na watu wanapotoka kuswali kuna kawaida ya kuzuru makaburi kwa ajili ya kuwasomea marehemu dua.
Kwa hapa nchini, sikukuu hii ya Idd itafanyika kitaifa katika eneo la Ugweno wilayani Mwanga Mkoani Kilimanjaro na huko ndipo kutakapokuwa na Baraza la Idd. Mgeni rasmi atakuwa Makamu wa Rais, Dk. Mohamed Gharib Bilal.
Mtume Muhammad (S.A.W) amewahimiza Waislamu kuhudhuria swala la Idd na hata kama mwanamke utakuwa kwenye hedhi basi akae pembeni watu waswali na wakishamaliza ajumuike nao kusikiliza hutba ya swala. Swala ya Idd huswaliwa uwanjani kwani hiyo ndio sunnah kutoka kwa Mtume.
Ili kusherehekea vizuri siku hii muhimu ni vema familia yaani baba, mama na watoto kwenda kuswali na kufuata yote yanayotakiwa ambayo nimeyaeleza. Ni vema kuepuka vitu ambavyo amevikataza Mungu katika siku hii kama kunywa pombe, kwenda disko, kucheza kamari na kufanya zinaa.

Wednesday, October 24, 2012

Polisi anaswa akiwania uongozi UVCCM

JESHI la Polisi Mkoa wa Dodoma, linamshikilia askari wake, F 7961 PC Stanley Mdoe wa Kituo cha Polisi Mvomero kwa tuhuma za kujihusisha na masuala ya siasa na kushiriki katika kinyang’anyiro cha kuwania ujumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (Nec) kupitia kundi la vijana.
Askari huyo pia anatuhumiwa kutumia ubini wa jina la Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Joel Bendera kama baba yake.
Habari  zilizopatikana kutoka mjini Dodoma zinadai kuwa askari huyo aliyejitambulisha kuwa yeye ni mtoto wa mkuu huyo wa mkoa, akijitambulisha kwa jina la Stanley Bendera, alikamatwa juzi jioni wakati wa uchaguzi wa viongozi wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), ukiwa unaendelea mjini Dodoma.
Kwa mujibu wa chanzo hicho, askari huyo akiwa amevalia sare za chama hicho tangu siku ya kwanza ya mkutano huo alikuwa akiomba wajumbe wa mkutano huo wampigie kura katika nafasi ya ujumbe wa Nec kupitia Mkoa wa Morogoro akiwa na wapambe wake ambao wengi wao walitokea mkoani humo.
Ilidaiwa kuwa askari huyo alikuwa amepamba gari lake kwa picha zake zilizokuwa zimeandikwa Stanley Joel Bendera jambo lililosababisha baadhi ya wanachama wa chama hicho wanaomfahamu kutoa taarifa kwa maofisa usalama waliokuwapo eneo hilo na Polisi Mkoa Dodoma ambao waliweka mtego wa kumkamata.
Mbali ya kukamatwa, askari huyo hakushinda katika nafasi hiyo. Awali, ilidaiwa kuwa askari huyo aliomba likizo isiyokuwa na malipo ili kupata fursa ya kushiriki uchaguzi huo.
Akizungumzia tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Faustine Shilogile alisema: “Sina taarifa ya askari huyo kujihusisha na siasa.”
Hata hivyo, Shilogile alisema alipata taarifa za kukamatwa kwake huko Dodoma akisema hata yeye alikuwa akimtafuta kwa shughuli za kikazi kwa siku mbili bila mafanikio.
Kamanda huyo alisema hana uhakika kuwa askari huyo amejiingiza katika siasa na kwa sasa ametuma askari wengine kufanya uchunguzi wa suala hilo.
Alisema endapo atabainika kujihusisha na siasa, atachukuliwa hatua za kinidhamu kulingana na taratibu za kijeshi.
Alisema endapo atathibitika kujihusisha na siasa, atakuwa amekiuka Katiba ya Tanzania Sura ya 9 inayokataza askari wa majeshi yote Tanzania kujihusisha na masuala ya siasa.
“Ni marufuku kwa mwanajeshi yeyote kujihusisha na masuala ya siasa na kwamba kama ni kweli amefanya hivyo ni kinyume na kanuni na taratibu za kazi,” alisema Shilogile.

RAIS MASIKINI ZAIDI DUNIANI

                                                       Rais Jose Mujica                        

NCHI ya Uruguay yenye raia takribani milioni 4, inatajwa kuwa na bahati ya kuwa na Rais asiye na chembe ya tamaa. Hana makuu, kiasi kwamba anatajwa kuwa ndiye Rais masikini zaidi kuwahi kutokea duniani.
Huyu si mwingine, bali ni Jose Mujica, Rais wa sasa wa Uruguay ambaye pia ni Rais wa 40 wa nchi hiyo. Tangu aingie madarakani Machi mosi mwaka 2010, amekuwa akionekana kuwa kiongozi wa tofauti kabisa, tofauti na waliomtangulia.
Mathalan, baada ya kufanikiwa kuishika nchini, hakuwa na tamaa ya kukimbilia Ikulu, yeye alichokifanya ni kuamua kuishi katika makazi yake yaleyale, katika nyumba ya mkewe iliyoko shambani, nje ya Jiji la Montevideo.
Kwa ujumla, anapenda maisha ya kawaida, maisha ya kuwahurumia wengine na kujitahidi kuonesha kwa vitendo.
Ni vigumu kuamini, licha ya kuwa ni Rais wa nchi, amejishusha mno kiasi cha mara kadhaa kuonekana akijichanganya na raia wake katika shughuli za ujenzi wa taifa, ikiwamo ujenzi wa barabara, kulima mashamba ya mfano.
Na wakati mwingine, anapougua huwahi kupanga mstari ili kuonana na daktari, akichelewa anapanga mstari kusubiri zamu yake.
Ni Rais pekee ambaye ameamua kutoa mshahara wake kwa zaidi ya asilima 90 kugawana na watu masikini wa nchi yake, kwamba fedha hizo huingizwa katika vikundi mbalimbali vya maendeleo.
Akiwa amepangiwa na Bunge kupokea dola za Kimarekani 11,000 (sh milioni 17.6 kwa fedha za Tanzania) kwa mwezi, hajawahi kupokea fedha hizo na ameiamuru Hazina kuzipeleka fedha hizo kwa wananchi masikini.
Yeye hupokea shilingi milioni 3 tu, tena hizi akizitumia kwa ajili ya mafuta ya gari lake alilonunua na mkewe aina ya Volkswagon Beetle maarufu kama `Mgongo wa Chura’. Gari hilo lenye umri wa miaka 23, ndio utajiri pekee anaojivunia.
Hana kingine anachokimiliki. Hana akaunti benki, hana nyumba yake binafsi, wala mali nyingine ya aina yoyote aliyojilimbikizia. Kuhusiana na gari lake lenye thamani ya dola za Kimarekani 1,900 (Sh milioni 3), ambalo analiendesha mwenyewe, anasema:
“Niko mimi na mke wangu, wawili tu, gari kubwa la nini, sina haja nalo, sitaki kuwaibia wananchi, kunichagua tu kuwaongoza ni sifa pekee, tena kubwa inayokaribia utukufu wa kawaida, sasa zaidi ya hapo nini…
“Nahitaji sana kuwatumikia wananchi wa Uruguay, sio kuwanyonya wala kuwaibia au kuwa mwanya wa kuchuma na kujifurahisha mimi, mke wangu, watoto wangu na ndugu zangu, sioni haja hiyo na sitaki kuwa mnyonyaji kamwe,” anasema Rais Mujica. Anasisitiza anayafurahia maisha ya kawaida, hivyo haoni shida kuishi na watu wa kawaida mtaani kwake, kupiga nao porojo na hata kushirikiana katika shughuli za kijamii pale inapolazimu.
“Nikiwa na akaunti benki, nikiwa na magari makubwa, nitakuwa nakaribisha ushawishi wa kuwa mwizi, kuwaibia wananchi wangu, sitaki chochote,” anaongeza Rais huyo ambaye hata anapoamua kunyoa nywele zake, hahitaji kinyozi maalumu, bali yeyote anayejua kunyoa anamwita nyumbani kwake aweze kumnyoa.
Staili ya maisha ya Rais huyo inaonekana pia kumwingia mkewe ambaye pia tofauti na wake wengine wa marais, yeye hajipambi kwa dhahabu, almasi wala aina nyingine ya vito vya thamani.
Anashirikiana na mumewe katika shamba lao la maua katika makazi yao, huku Rais Mujica wakati mwingine akifanya usafi wa nyumba na hata kumwagilia maua. Hayo ndiyo maisha ya Jose Mujica, Rais wa 40 wa Uruguay ambaye kwa sasa ana umri wa miaka 77, lakini licha ya kupigania mno kuingia Ikulu, ameonesha kutokuwa na kiu ya utajiri, hataki kujikweza na wala kuonekana ni tofauti na watu wengine.
Ndiyo maana ameonekana kuwa Rais wa ajabu, akitajwa pengine kuwa ndiye asiye na makuu na masikini kuliko wote duniani. Hata vaa yake ni ya kawaida, mara nyingi akiingia ofisini na mavazi ya kawaida, lakini mara moja moja tu, akivalia suti na tai hasa anapokuwa na ugeni mzito.
Angalau Makamu wake, Danilo Astori anaonekana na `ufisadi’ kidogo, kwani ana nyumba yenye thamani ya dola 250,000 (Sh milioni 400) na gari kama la milioni 30 hivi. Je, kuna wengine wenye staili ya maisha ya Rais Mujica? Yawezekana, lakini kwa sasa imeonekana hakuna kama Mujica.

Sunday, October 21, 2012

SERIKALI: MIHADHARA YA DINI MARUFUKU


                                   Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi                                               

Serikali imepiga marufuku mihadhara yote inayochochea vurugu za kidini na kutangaza kuwakamata wote wanaofadhili vikundi hivyo.

Tamko hilo limetolewa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi  wakati akizungumza na waandishi wa habari jana, jijini Dar es Salaam.

Alikuwa akizungumzia matukio ya vurugu zilizofanywa na baadhi ya watu wanaoaminika kuwa Waislamu katika miji ya Zanzibar na Dar es Salaam, yaliyotokea  juzi.

Alisema mihadhara yote ya kidini imepigwa marufuku kwa muda wa mwezi mmoja huku serikali ikifanya  uchunguzi ili kubaini watu wanaofadhili vurugu hizo kutoka nje na ndani ya nchi.

Dk. Nchimbi alisema Serikali imejipanga kuhakikisha inatumia nguvu pamoja na vyombo vya sheria endapo itabaini kuna dalili ya watu kufanya mipango ya kuanzisha vurugu kwa kisingizoa cha dini.

"Serikali tumechua maamuzi mapya kuhusu suala kama hili, hapo mwanzo tulikuwa tunawakamata wale wanaoshiriki lakini sasa tutawakamata wale wote waliofanikisha, waliotekeleza na waliowatuma," alisema waziri Dk. Nchimbi.

Alisema uamuzi huo wa Serikali umechukuliwa kwa nia njema ya kutetea nchi isitumbukizwe katika vita vya kidini na watu wachache ambao aliwaita ni wahuni.

Alisema chanzo cha vurugu zilizofanyika Zanzibar na Dar es salaam hazina msingi wowote kwa sababu madai yaliyotolewa na watu wa Kikundi cha Uamsho kwa Zanzibar na Jumuiya za Taasisi za Kiislamu  kwa Tanzania bara hazina msingi na Serikali hausiki.

KIONGOZI WA UAMSHO ASHIKILIWA NA POLISI

Waziri Dk. Nchimbi alisema Jeshi la Polisi linamshikilia Kiongozi wa Kikundi cha Uamsho Sheikh Farid Hadi  kwa mahojiano ili ataje mahali alipokwenda baada ya kutoweka siku kadhaa na kusababisha wafuasi wake kufanya vurugu katika mitaa mbalimbali ya mji wa Zanzibar.

Alisema Serikali haikuhusika na kutoweka kwa kiongozi huyo ndio maana imeamua kumshikilia ili aeleze wapi alikuwa siku hizo, nia na madhumuni ya kutoweka huko.

"Kama mtu alitoweka ghafla na baadae anaonekana akinywa kahawa lazima Serikali ishtuke, tumeona lazima tumshikilie kwa mahojiano ili atuambie alikuwa wapi, nia ya kutoweka na madhumuni yake ili  umma uelewe," alisema Dk. Nchimbi.

Alisema Tanzania inaendeshwa kwa mujibu wa sheria na hakuna mtu ambaye hawezi kuguswa kwa kuhofia watu kufanya vurugu.

"Hatutabembelezana tena jambo kama hili, tufuate sheria na hakuna mtu ambaye atakuwa haguswi, tutamgusa na wale watakaoleta vurugu tutapambana naye," alisisitiza.

SHEIKH PONDA KAMWE HAACHIWI KWA MAANDAMANO.

Akizungumzia kuhusu suala la Sheikh Issa Ponda, Dk Nchimbi alisema wanaoleta vurugu kwa kushinikiza Sheikh Ponda kuachwa huru wamegonga ukuta kwa sababu tayari yupo katika mikono ya mahakama na hakuna mtu atakayeweza kumtoa nje.

Alisema kwenye vurugu zilizotokea jijini Dar es Salaam, baadhi wa wafuasi wake walikuwa wakiishinikiza Serikali kumtoa nje kiongozi huyo jambo ambalo kamwe halitawezekana.

Alisema kimsingi mahakama ndio yenye mamlaka ya kufanya hivyo kutokana na mipaka ya kiutendaji iliyopo kikatiba.

"Madai yao hayana msingi kwa sababu Sheikh Ponda amefikishwa mahakamani na hakuna mtu anayeweza kuingilia mahakama, wasubiri siku iliyopangwa kusikilizwa na kwa kesi hiyo pengine anaweza kuomba na kupewa dhamana," alisema.

NCHI IPO HATARINI

Hata hivyo Waziri Nchimbi alisema Watanzania wasikubali kuona watu wanataka kuweka nchi katika mpasuko wa kidini na kusababisha kuwepo kwa mauaji ya halaiki.

Alisema Serikali haitakubali kuona nchi inapoteza amani na utulivu uliojengwa kwa nguvu kubwa na waasisi wake Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere na Aman Karume kwa sababu vizazi vinavyokuja vitakuja kuwahukumu.

Alisema jukumu la Serikali iliyowekwa madarakani na wananchi kidemokrasia ni kuhakikisha nchi inakuwa tulivu na yenye amani, hivyo aliwataka wananchi wote kuunga mkono hatua zote za Serikali zitakazochukua katika kufanya wananchi wote wanaishi kwa udugu na ushirikiano kama zamani.

Dk Nchimbi alisema Serikali ipo tayari kukaa pamoja na vikundi mbalimbali vya kidini, taasisi na mashirika yasiyo ya kiserikali kujadili jambo hilo, lakini haipo tayari kufanya mazungumzo kwa shinikizo la mtu.


source: ippmedia