TUME ya Haki za Binadamu na Utawala Bora
imesema wakati kuna madai kwamba Jumuiya ya Uamsho ni ya kidini
(Kiislamu), lakini imekuwa ikitumiwa na makundi ya wahuni ambayo
yamejipachika majina tofauti.
Taarifa ya Tume hiyo iliyotumwa kwa
vyombo vya habari jana ikiwa imesainiwa na Kamishna wake, Zahor Khamis,
imetaja baadhi ya majina ya makundi hayo kuwa ni Mbwa mwitu, Simba
mkali, Ubaya ubaya na Toto tundu na kuongeza kuwa yamekuwa yakitumika
kufanikisha azma yao.
Mbali na jumuiya hiyo kutumiwa na
wahuni, Tume pia imesema kutekwa kwa kiongozi wa jumuiya hiyo, Shekhe
Farid Hadi Ahmed, kuna utata mkubwa ambao unahitaji uchunguzi na
ufafanuzi kufahamu huko alikotekwa na kutoa mfano wa madai ya kunyimwa
kula kwa siku tatu bila kuathirika kiafya.
Tume hiyo imehoji kama kweli alikuwa
ametekwa, aliwezaje kufika msalani ambako alikuwa akinywa maji, wakati
alikuwa amefungwa kitambaa usoni na mikononi akiwa na pingu na ilikuwa
nyumba ambayo haijui! Kutokana na utata huo, Tume imemtaka Shekhe Farid
kutoa maelezo yanayothibitisha pasipo shaka ili kuwathibitishia
Wazanzibari, Watanzania na ulimwengu kwa jumla, juu ya kutoweka kwake.
“Shekhe Farid amedai alitekwa na watu
wasiojulikana tarehe 16 mwezi huu na kuonekana siku tatu baadaye akiwa
katika hali ya uzima na salama jambo ambalo lilisababisha vurugu kubwa
Zanzibar na kusimama kwa shughuli zote za kiuchumi na kijamii,” ilieleza
taarifa hiyo ya Tume.
Kwa mujibu wa Tume, kutokana na fujo
hizo zilizotokea, hasara ilitokea ambayo mpaka sasa haijajulikana
thamani askari Polisi wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), Said
Abdulrahman kuliuawa.
Kutokana na matukio hayo, Tume
imeishauri Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, kuwatafuta na kuwakamata wote
walioshiriki katika vurugu hizo na kuvunja vikundi vyote vya kihalifu
vilivyoanza kushamiri Zanzibar.
“Tunalaani mauaji ya askari Abdulrahman
kwani ni uvunjaji wa haki za biaadamu, inapingana na sheria za nchi na
ni kinyume na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ibara ya 14
inayozungumzia haki ya kuishi na Katiba ya Zanzibar ibara ya 13
inayozungumzia haki ya kuwa hai,” taarifa hiyo ilifafanua.
Tume pia imelaani kitendo alichofanyiwa
Diwani wa CCM Wadi ya Chumbuni kwa kushambuliwa na kujeruhiwa, kitendo
ambacho kinakwenda kinyume na haki za binaadamu na Katiba ya Tanzania
inayopiga marufuku mtu kuteswa, kuadhibiwa kinyama au adhabu za
kumdhalilisha.
“Kuna uhusiano gani wa kutekwa kwa
kiongozi wa Uamsho na hujuma za mali za watu na CCM?” Taarifa hiyo
ilihoji. Kwa mujibu wa Kamishina wa Jeshi la Polisi Zanzibar Mussa Ali
Mussa Polisi inafanya uchunguzi wa kina kubaini kama Shekhe Farid
anahusika na mtandao hatari wa ugaidi wa Al-Qaeda.
Akizungumza na gazeti hili kwa simu
jana, Mussa alisema Polisi nchini inafanya kazi hiyo kwa kushirikiana na
taasisi za kimataifa ikiwamo Polisi - Interpol.
“Jeshi la Polisi nchini kwa sasa
linafuatilia kwa karibu sana nyendo zote za kiongozi wa Uamsho Shekhe
Farid ikiwamo kuhusishwa kwake na mtandao wa Al-Qaeda,” alisema.
0 comments:
Post a Comment