SIKU ya leo wengi wetu tumezoea kuiita sikukuu kubwa tukisema ni siku
ambayo wakubwa ndiyo wanapewa zawadi na pia tumezoea kusoma ni sikukuu
ya Mfungo tatu.
Sikukuu hii kubwa ina majina mengi kiasi, ambayo ni Idd el Hajj yaani
Idd ya Hijja; Idd al Adh-ha yenye maana sikukuu ya sadaka lakini pia
inafahamika kama Idd la Kabir ambayo ni sikukuu kubwa. Sikukuu hii
hupatikana katika mwezi huu wa kiislamu unaofahamika kama Dhul Hijjah
ambao ni mwezi wa Hija na ni mtukufu.
Katika mwezi huu kuna siku 10 za mwanzo ambazo ni siku bora kabisa
katika dunia na zina fadhila kubwa kutokana na aya na hadithi
mbalimbali.
Miongoni mwa hadithi ni ile inayotokana na Ibn Abbas (Radhiya Lahu
anhuma). Mtume wa Mwenyezi Mungu (S.A.W) amesema: “Hakuna siku ambazo
vitendo vyake vyema anavipenda Allah kama siku kumi hizi (siku kumi za
mwanzo wa mwezi wa Dhul-Hijja).
Akaulizwa je, hata Jihaad katika njia ya Allah? Akajibu “hata jihaad
katika njia ya Allah isipokuwa mtu aliyekwenda na maisha yake na mali
yake ikawa hakurudi na kimojawapo”.
Vitendo hivyo vyema vinavyotajwa ni pamoja na kutimiza Hijja na Umra
kwa wenye uwezo; kuomba toba ya ukweli; Kufunga siku hizi hasa siku ya
Arafah; kuzidisha vitendo vyema mbalimbali kama kuswali sunna zaidi,
kusoma Kurani, sadaka, dua, kutii wazazi, kuwasiliana na jamaa, kufanya
wema na jirani, kuambizana yaliyo mema na kukatazana yaliyo maovu,
kufanyiana wema na ihsani na kuchinja baada ya swala ya Idd.
Pia kumkumbuka sana Allah (S.W) kwa Tasbih, Tahmid, Tahlil na Takbir
ambayo ni “Allahu Akbar, Allahu Akbar, Laa Ilaha Illa Allaah Wa-Allaahu
Akbar, Allahu Akbar Walillahil-hamd”.
Takbir inapaswa kusomwa wakati wote usiku au mchana tokea unapoingia
mwezi wa Dhul-Hijja na inaendelea mpaka siku ya mwisho ya siku za
Tashriq na pia baada ya kila swala na huanza asubuhi ya siku ya Arafat
mpaka siku ya mwisho ya Tashriq .
Siku ya 11, 12 na 13 ya Dhul-Hijja yaani baada ya siku ya Idd
zimeitwa siku za Tashriq kwa sababu watu walikuwa wakikatakata nyama na
kuzianika juani. Pia siku hizi hujulikana kuwa ‘siku za Minaa’.
Inatakiwa Wanaume waseme Takbir kwa sauti ili kuwakumbusha wengine
kurudisha sunna ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (S.A.W) na wanawake waseme
kimya kimya isipokuwa wakiwa na mahaarim wao.
Imesemekana kuwa ukiandama mwezi wa Dhul-Hijja Ibn ‘Umar na Abu
Hurayrah walikuwa wakienda sokoni na kufanya takbir kwa sauti ili
kuwakumbusha watu.
Nikirudia siku hii ya Idd ambayo huitwa ya sadaka ni kutokana na watu
kutakiwa kuchinja mnyama kama mbuzi, ng’ombe au kondoo na kisha kutoa
sadaka kwa masikini na pia kutumiwa katika familia na ndiyo sababu kwa
watu waliokwenda Makka kuhiji kuchinja wanyama.
Baada ya kuchinja kama alivyoagiza Mtume Muhammad (S.A.W), mchinjaji
anaamrishwa aigawe nyama mafungu matatu, fungu moja awape masikini na
mafakiri , fungu la pili awape majirani na ndugu na lile la tatu ni lake
na familia yake.
Uchinjaji huu ni kama kumbukumbu ya sadaka ya Nabii Ibrahim ambaye
anatajwa kwenye Kurani na Biblia kuwa alikuwa tayari kumchinja mwanawe
wa kumzaa Nabii Ismail kama kwenye Kuran au Isaka (Biblia) kama sadaka
kwa Mwenyezi Mungu lakini Mungu alimzuia asimchinje na akampatia
mwanakondoo badala yake.
Mafundisho yanatueleza kuwa malaika Jibril alimshika mkono nabii
Ibrahim kabla ya kumchinja mtoto wake Ismail ikiwa ni ishara ya kumzuia
kutenda tendo hilo na ndipo aliposhushiwa kondoo amchinje. Maelezo hayo
yanapatikana katika Kurani kwenye sura ya al-Hajj aya ya 37 na Biblia
katika kitabu cha Mwanzo sura ya 22 ambapo anatajwa kama Abraham.
Uchinjaji huo wa mnyama unafanyika baada ya swala ya Idd ambapo Allah
(S.W) amesema katika suratul Kawthar 108:2 “Basi swali kwa ajili ya
Mola wako na uchinje “. Ibada hii ya kuchinja ni sunna iliyosisitizwa
hata na baadhi ya wanazuoni ambao wameona kuwa ni wajibu kwa kila
aliyekuwa na uwezo.
Muislamu kabla ya kufikia hatua ya kuchinja anatakiwa kutia nia ya
kuchinja, asikate nywele wala kucha mpaka amalize kuchinja. Kuna hadithi
moja inasema: “Ukiandama mwezi wa Dhul-Hijja na ikiwa yuko anayetaka
kuchinja basi asikate kucha wala nywele wala kutoa kitu katika ngozi
yake mpaka akimaliza kuchinja”.
Idd husherehekewa kati ya tarehe 10 hadi 13 ya mwezi wa Dhul Hijjah
wa kalenda ya Kiislamu. Tarehe halisi hutegemea kuonekana kwa mwezi. Kwa
mwaka huu ndiyo siku ya leo ambayo ni siku nzuri ya Ijumaa. ]Sherehe za
siku hii huanza kwa swala la Idd na baadaye kufuatiwa na baraza la Idd
na watu wanapotoka kuswali kuna kawaida ya kuzuru makaburi kwa ajili ya
kuwasomea marehemu dua.
Kwa hapa nchini, sikukuu hii ya Idd itafanyika kitaifa katika eneo la
Ugweno wilayani Mwanga Mkoani Kilimanjaro na huko ndipo kutakapokuwa na
Baraza la Idd. Mgeni rasmi atakuwa Makamu wa Rais, Dk. Mohamed Gharib
Bilal.
Mtume Muhammad (S.A.W) amewahimiza Waislamu kuhudhuria swala la Idd
na hata kama mwanamke utakuwa kwenye hedhi basi akae pembeni watu
waswali na wakishamaliza ajumuike nao kusikiliza hutba ya swala. Swala
ya Idd huswaliwa uwanjani kwani hiyo ndio sunnah kutoka kwa Mtume.
Ili kusherehekea vizuri siku hii muhimu ni vema familia yaani baba,
mama na watoto kwenda kuswali na kufuata yote yanayotakiwa ambayo
nimeyaeleza. Ni vema kuepuka vitu ambavyo amevikataza Mungu katika siku
hii kama kunywa pombe, kwenda disko, kucheza kamari na kufanya zinaa.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments:
Post a Comment